Skip to main content

      MTWANGAJI




01:Nianze na wa nyumbani, salamu kuwatolea

Jamani mu hali gani, zipoje zenu afia

Nanyi wa ughaibuni, amani nawatakia

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.

 

02:Niwajuze yangu fani, kwa dhati nilobobea

Si fundi wa cherehani, dereva na abiria

Wala ticha darasani, zote sijazizoea

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.

 

03:Si nguvu bali akili, ndio ninayotumia

Kinu ninakikabili, mtwangio kushushia

Mimi fundi kwelikweli, kutwanga nimebobea

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.

 

04:Nikiziona nafaka, zimetulia kinuni

Unanipanda wahaka, nasisimuka mwilini

Mchi mate naupaka, tayari nipo kazini

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.

 

05:Tena kutwangia kinu, kisikalie pembeni

Zisije kufeli mbinu, mchi ukatwanga chini

Kina mwajuma na tunu, wanione punguani

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.


06:Ukitua mtwangio, kusaga hizo nafaka

Hubakia mshangao, kinu kina taabika

Nakaa kila mkao, ufaao kutwangika

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.

 

07:Umakini naongeza, ninapotwanga kinuni

Natwanga na kupuliza, kwa kati na ukingoni

Nafaka zisijecheza, nikamwagia pembeni

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.

 

08:Ya utwanzi kazi yangu, siifanyi hadharani

Mimi sifinyangi chungu, kwamba nikae juani

Najificha ndani kwangu, nafaka natwanga ndani

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.

 

09:Tam tam yangu kazi, mwenyewe nimeridhika

Nahema kwa kasi pumzi, ninapoanza kuchoka

Ninatwanga kwa mapozi, kijasho kikinitoka

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.

 

10:Zinapoiva nafaka, mtwangio nautoa

Kinu maji nakipaka, kesho nije kitumia

Moyoni nafurahika, kazi imeshatimia

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.

 

11:Kufanya nyengine kazi, hilo wazo na likome

Sibadili maamuzi, wacha roho ziwaume

Nitazidisha ujuzi, najiamini kidume

Naringia mtwangio, unaniweka mjini.

 

 

MTUNZI:HUSSEIN.R.KAPARATA

TEL:0714631510

huseinkapa112@gmail.com


Comments

Popular posts from this blog

                    MLAJI 1;Enyi walaji wa leyo, kusema nanyi nataka Ipunguzeni pupiyo, lasivyo mtadhurika Nyoyo zipeni zuiyo, mwili utabusarika Shikilia wako moyo, mlaji utaumia.   2;Mnapopita shambani, matunda yawazuzuwa Mboga hamzitamani, zawachosha kuchambuwa Macho yote yamtini, paku mnaupekuwa Shikilia wako moyo, mlaji utaumia.   3;Muonapo tunda pera, limelala kidarini Nyanyachungu ama tura, mbili mbili zi tawini Kwa kebehi mnafura, mwasema hizi za nini Shikilia wako moyo, mlaji utaumia.   4;Mwataka ulojazia, mti hadi mashinani Ili ukiupandia, uhisi u kitandani Huku dodo wajilia, wajipea burudani Shikilia wako moyo, mlaji utaumia.   5;Muonapo ni papai, au dodo mwalichuma Mwajitia ubedui, kulipapasa kwa nyuma Kifuatacho jimai, kichwani mwawaza nyama Shikilia wako moyo, mlaji utaumia.   6;Kisha hufata vurugu, za kwichi kwichi mtini Yale mavuno ya njugu, mli...
            BWANA DHIKI 1;Hana baba wala mama,wala ndugu wa kunusa Halali ndani ya hema,jua mvua yamtosa Ngozi yake ya ukoma,ngumu kwa kuipapasa Wamuita bwana dhiki,jinale yake maisha.   2;Hana kazi wala bazi,anafanya dei waka Elimu hana ujuzi,darasani hakufika Machinga na wachuuzi,humfanya kibaraka Wamuita bwana dhiki,jinale yake maisha.   3;Kuu kuu nguo zake,mabwende yalotoboka Waume kwa wanawake,husema amechizika Upitapo kando yake,uvundo unamnuka Wamuita bwana dhiki,jinale yake maisha.   4;Sura yake ni nyeusi,tii yenye kupauka Mfupi kama kipisi,ama shina la mugoka Mapele kama fenesi,ngoziye imebabuka Wamuita bwana dhiki,jinale yake maisha.   5;Watupavyo jalalani,vyote vilo haribika Ndizi mboga za majani,na nyama zinazo nuka Hushindilia tumboni,haogopi kudhurika Wamuita bwana dhiki,jinale yake maisha. 6;Yupo peku miguuni,kokoto zinamng'ata Apitapo jalalani,vigae v...