BWANA DHIKI
1;Hana baba wala
mama,wala ndugu wa kunusa
Halali ndani ya
hema,jua mvua yamtosa
Ngozi yake ya
ukoma,ngumu kwa kuipapasa
Wamuita bwana
dhiki,jinale yake maisha.
2;Hana kazi wala
bazi,anafanya dei waka
Elimu hana ujuzi,darasani
hakufika
Machinga na
wachuuzi,humfanya kibaraka
Wamuita bwana
dhiki,jinale yake maisha.
3;Kuu kuu nguo
zake,mabwende yalotoboka
Waume kwa
wanawake,husema amechizika
Upitapo kando
yake,uvundo unamnuka
Wamuita bwana
dhiki,jinale yake maisha.
4;Sura yake ni
nyeusi,tii yenye kupauka
Mfupi kama
kipisi,ama shina la mugoka
Mapele kama
fenesi,ngoziye imebabuka
Wamuita bwana
dhiki,jinale yake maisha.
5;Watupavyo
jalalani,vyote vilo haribika
Ndizi mboga za
majani,na nyama zinazo nuka
Hushindilia
tumboni,haogopi kudhurika
Wamuita bwana
dhiki,jinale yake maisha.
6;Yupo peku
miguuni,kokoto zinamng'ata
Apitapo
jalalani,vigae vinamsuta
Augulia
rohoni,maumivu anopata
Wamuita bwana
dhiki,jinale yake maisha.
7;Mwanzo alilia
sana,hadi kwikwi kumtoka
Sasa
ametulizana,machozi yamekauka
Wakumjali
hakuna,lau angeimarika
Wamuita bwana
dhiki,jinale yake maisha.
8;Macho
wamemfumbia,wenye vikubwa vitambi
Viziwi
wanajitia,wazidisha na vitimbi
Eti
ameyazoea,maisha ya kula vumbi!
Utu wa mtu ni
utu,musiupime kwa kitu.
9;Kwa fujo
wanampita,ndani ya yao magari
Wazidi kukunja
ndita,kwake hawana habari
Watupacho
aokota,mola kampa nusuri
Utu wa mtu ni
utu,musiupime kwa kitu.
10;Angalikuwa na
baba,ama japo familia
Asinge pata
suluba,nafuu ingemjia
Dunia inamkaba,hana
wa kumtetea,
Utu wa mtu ni utu,
musiupime kwa kitu.
11;Kaparata
najivika,joho la kumtetea
Nahisi hapa
patosha,mkome kumkandia
Kula kwa kurasha
rasha,ni dhiki hakuzoea
Utu wa mtu ni
utu,musiupime kwa kitu.
12;Zifikisheni
habari,kwa mandusa na vitambi
Wasijipe
ujabari,wa kuhalalisha dhambi
Wakanye kwa
tahadhari,vikome vyao vitimbi
Utu wa mtu ni
utu,musiupime kwa kitu.
13;Kama kuandika
sumu,adhabu inikabili
Silaha yangu
kalamu,kuondosha idhilali
Sababu yalo
haramu,kuyaacha ni muhali
Utu wa mtu ni utu,musiupime
kwa kitu.
*MWISHO*
Mtunzi:Hussien.R.Kaparata
TEL.0714631510

Comments
Post a Comment